BARAZA LA WAWAKILISHI SPORT CLUB YATOKA SARE YA 1-1 NA MADIWANI WA MAGHARIBI “B”.

Posted on: 19.05.2026

Timu ya mpira wa miguu ya Baraza la Wawakilishi Sport Club imefanikiwa kutoka sare ya bao 1-1 na Timu ya Madiwani wa Wilaya ya Magharibi “B” uliochezwa katika Uwanja wa Kitogani.

Katika mchezo huo wa kirafiki ,Timu ya Baraza la Wawakilishi Sport Club iolionesha kujipanga vyema kutokana na kuonesha umoja wa hali ya juu katika kuumiliki mpira na kutafuta nafasi za kutoka katika kuzishambulia nyavu za Timu ya Madiwani.

Goli la Timu ya Baraza la Wawakilishi lilifungwa na Mhesimiwa Ali Abdulghulam Hussein ambae pia ni Naibu Waziri wa Habari, Sanaa, Utamaduni na Michezo baada ya kupokea pasi safi kutoka kwa Mheshimiwa Mmanga Mohammed Hamed (Jimbo la Tumbe).

Mwenyekiti wa Baraza la Wawakilishi Sport Club Mhe. Mahfoudh Abdalla Mohammed amesema ameridhishwa na kiwango kikubwa walichokionesha wachezaji wake kwa vile ni mechi yao ya Kwanza tangu kuanza kwa Baraza la 11 la Baraza la Wawakilishi.

Hata hivyo Mhe. Mahfoudh amewahimiwa wachezaji wa Timu ya Baraza la Wawakilishi Sport Club kuendelea na mazoezi ili kuwa na afya njema pamoja na kuendelea kufanya vizuri zaidi katika mechi zijazo.

Kepteni wa Timu hiyo Mhe. Khamis Mohammed Amrani (Jimbo la Mkoani) amesema lengo la Timu ya Baraza la Wawakilishi Sport Club imeamua kucheza mechi hiyo ili kujenga mahusiano mazuri na ukaribu zaidi na Wawakilishi katika sekta mbali mbali ikiwemo michezo.

Mgeni rasmi katika mchezo huo alikuwa ni Naibu Spika wa Baraza la Wawakilishi Mhe. Mwanaasha Khamis Juma.                                              

//